Tuesday, April 22, 2014

WAZIRI MBENE AHAMASISHA UWEKEZAJI EPZA

SERIKALI imewahamasisha wawekezaji wa ndani na nje kuwekeza kwa wingi katika maeneo ya Mamlaka ya Ukanda Maalumu wa Uwekezaji nchini (EPZA) kwa faida yao na ya nchi kwa ujumla.
Naibu Waziri wa Viwanda na Biashara, Janeth Mbene, alisema uwekezaji katika maeneo hayo una uwezo mkubwa wa kuongeza uzalishaji wa bidhaa kwa masoko ya nje na hivyo kukuza uchumi wa nchi kwa haraka.
Waziri huyo alitoa kauli hiyo jijini Dar es Salaam mwishoni mwa wiki alipotembelea Kiwanda cha Tanzania Tooku Garments Co. LTD kilichopo eneo la EPZA.
“Maeneo haya yana fursa nyingi ambazo wawekezaji wanaweza kufaidika nazo…nawahamasisha waje kwa wingi na serikali itawasaidia kuweka mazingira bora zaidi,” alisema Mbene.
Kiwanda hicho kinatengeneza nguo kwa ajili ya soko la nje ya nchi.
“Nina furahi kuona kiwanda hiki kimetoa ajira kwa Watanzania wengi…haya ndiyo mambo ambayo serikali inapigania wakati wote,” alisema.
Kabla ya kufanya ziara katika kiwanda hicho, naibu waziri huyo alikutana na watendaji wa EPZA na kufanya nao mazungumzo.
Katika mazungumzo yao, aliwahakikishia watendaji na viongozi wa mamlaka hiyo kuwa serikali itaendelea kushirikiana nayo katika kusukuma gurudumu la maendeleo.
Meneja Mkuu Msaidizi wa Tanzania Tooku Garments Co Ltd, Rigobert Massawe, alisema kiwanda hicho kinazalisha nguo aina ya jeans na tisheti kwa ajili ya masoko ya nje.
Alisema kwa sasa wanatumia zaidi soko la Marekani na baada ya maboresho zaidi watauza katika soko la Uingereza.
Kwa mujibu wa Meneja huyo, kiwanda kimeajiri Watanzania zaidi ya 800 na  kinatarajia kufikia mwaka 2025 kitaweza kuajiri watu 15,000.
Akizungumza hivi karibuni, Mkurugenzi Mkuu wa mamlaka hiyo, Dk. Adelhelm Meru, alisema mamlaka yake imedhamiria kuona uwekezaji unakua na kuchangia maendeleo ya nchi hasa kupitia viwanda.

No comments:

Post a Comment